JE, UNAZIJUA DAWA HATARI KWA POMBE ??

Zifahamu dawa hatari kutumia pamoja na pombe.

Pombe ni nini hasa ?

Habari yako ndugu mpenzi msomaji wa blog yako ya “ZIJUE DAWA ZAKO”, pia pole na majukumu ya kila siku. Leo napenda kukuletea ya dawa iitwayo “Pombe”. Pombe ni kundi la kemikali mbali ambazo namna au nyingine zinafanana kwa matokeo yake, kundi hili linahusisha kemikali kama (majina ya kitaalamu) Ethanol, Methanol na ethyl glycol. Ethanol ndio inapatikana kwa wingi katika vileo vingi. Natumaini ulishawahi kukutana na maelekezo yakitolewa na mfamasia au daktari kwamba usitumie pombe kabisa hadi pale utakapo utakapomaliza dozi yako, basi karibu tena leo uzijue dawa ambazo hutakiwi kutumia pombe kabisa ukiwa kwenye dozi.

   Najua utashangaa kwanini pombe nimeiita ni dawa, labda nieleze kidogo kwanini nimeiita pombe kuwa ni dawa, Pombe ni dawa kwa sababu, utendaji kazi wake ni sawa kabisa na jinsi ambavyo dawa za usingizi hufanya kazi. Madhara yake baadhi pia nayo yanafanana na dawa za usingizi. Na pia Pombe aina ya ethanol hutumika kusafishia vidonda, kusafisha mikono baada ya kusafisha majeraha na kusafishia vifaa kwa minajili ya kuua vimelea vyovyote ambavyo vyaweza kuwepo pale.
   Hebu sasa tuangalie dawa ambazo hutakiwi kutumia kileo au pombe yoyote uwapo kwenye dozi, Dawa hizi ambazo tunaenda kuziona hapo chini husababisha madhara ambazo zinajidhihirisha kupitia dalili zifuatayo kama zikitumiwa pamoja na pombe; Kichefuchefu, kutapika, kizunguzungu, maumivu ya kichwa na Joto na kujaa usoni. Dalili hizi zinaweza kusababisha kifo kama mgonjwa hatawahishwa hospitali kwajili ya kuzishughulikia.

1.      DISULFIRAM, METRONIDAZOLE, TRIMETHOPRIM NA CEFOTETAN.

Dawa hizi hutumika kutibu matatizo (Magonjwa) mbalimbali ya mwili zikiwa katika muunganiko na dawa zingine au pekee. Magonjwa yanatibiwa na hizi dawa ni kama yafuatayo kwa ufupi,

·         Disulfiram

 Dawa hii hutumika kutibu saratani inayotokea kwenye mishipa ya fahamu sehemu ambazo kitaalamu zinaitwa ganglia. Saratani hii inaitwa Glioblastoma Multiforme.

·         Metronidazole

Metronidazole ni jina la dawa husika ambayo imezoeleka kuitwa kwa jina la flagyl, Dawa hii husaidia au hutibu magonjwa yanayosababishwa na wadudu waitwao bakteria. Na pia dawa hii hutumika kuzuia mambukizi kwa wagonjwa wanaojiandaa kwajili ya operesheni na hata baada ya operesheni hutumika.

·         Trimethoprim

Hii dawa hupatikana katika muunganiko au pekee ake. Katika muunganiko wa dawa hii inajulikana kwa jina la septirini, natumaini hili jina sio geni kwako. Dawa hii hutumika kutibu UTI na magonjwa yanasababishwa na wadudu kwenye mfumo wa hewa. Magonjwa kama niumonia.

·         Cefotetan

Hii dawa hutumika Kama dawa ya kuua wadudu waitwao bakteria wanaopatikana mwilini, dawa hii hutumika katika mazingira mbalimbali ikiwemo kuzuia kuingia au kusambaa Kwa wadudu kwa magonjwa anayeandaliwa kwajili ya operesheni au baada ya kutoka kwenye operesheni. Mbali na hayo, dawa hii hutumika kutibu magonjwa yasababishwayo na wadudu wafuatao; Bacteroides spp., C.perfringes, E.coli, H.inflenze na N.gonorrhoeae. Kiujumla dawa hii hutibu magonjwa yasababishwayo na jamii ya wadudu walioko kwenye kundi lijulikanalo kitaalamu kama gram negative (-ve) na gram positive (+ve).


2.      DAWA ZA KUTIBU MIWASHO NA DALILI ZOZOTE ZINAZOHUSIANA NA ALEJI. 

Dawa nyingi (sio zote) zinazotumika kuondoa au kutibu matatizo yoyote yanayohusiana na aleji, utendaji kazi wake huhusisha hadi mfumo wa kati wa fahamu (ubongo) kwa kitaalamu unaitwa central nervous system (CNS). Moja ya madhara yanayosababishwa na hizi dawa ni kupunguza uwezo na umakini kwenye ufanyaji kazi wa ubongo hivyo kusababisha dalili kama vile usingizi na kupungua kwa ufanisi kwenye kazi. 

 Hivyo basi, kwasababu pombe nayo husababisha madhara yanayofanana na yale ambayo yanasababishwa na dawa za kutibu aleji au miwasho yoyote (Anti-allergy), kwahyo kutumia pombe pamoja na hizi dawa inaongeza hatari ya kupunguza utendaji kazi wa ubongo na hata inaweza kupelekea madhara hatari zaidi kama vile kupoteza fahamu au kuzimia.

Dawa zifuatazo ndio zinazotumika kutibu au kuondoa miwasho mwilini, mpangilio wa orodha hii ya dawa za kutibu aleji umewekwa kwa mtindo kupungua uwezo wa kusababisha madhara yaliyotajwa hapo juu. Orodha yenyewe ni kama ifuatayo;
·         Bronpheniramine
·         Chorpheniramine (piritoni)
·         Ciproheptadine
·         Diphenhydramine
·         Doxylamine
·         Promethazine
·         Acrivastine
·         Cetirizine
·         Levocetirizine
 Hivyo basi, ni jambo la muhimu sana kujiepusha na pombe uwapo katika dozi inayohusisha dawa moja au mbili zilizotajwa hapo huu. Pamoja na hayo, pombe imehusishwa na kusababisha kuharibika au kupungua kwa utendaji kazi wa ini ambalo linashughulika na uvunjaji wa dawa na sumu zote zinazoingia mwilini. Hivyo basi, utumiaji wa pombe kwa muda mrefu unaweza kusababisha kukusanyika kwa kiasi au kiwango cha sumu mwilini kitu ambacho kinaweza kusababisha madhara makubwa zaidi mwilini na hata kusababisha madhara kwenye viungo vingine kama figo. Hivyo basi uwapo katika dozi ya dawa yoyote ni vyema kupunguza kuacha kabisa unywaji wa pombe hadi umalize dozi yako.
  Pia pombe inauwezo wa kuchochea uvunjaji wa dawa mwilini (enzyme inducer), uvunjaji huu wa dawa unapochochewa unapelekea kupungua kwa kiwango cha dawa kinahitajika kusababisha matokeo chanya kwenye kutibu matatizo mbalimbali ya mwili.
 Basi, ni jambo jema na la busara kumshirikisha mfamasia au daktari aliyekuhudumia ili akupatie maelezo au tahadhari zozote zinazohitajika kuzifahamu wakati wa kutumia dawa na pombe ili kuzuia madhara yanayoweza kujitokeza baada ya kutumia. Ahsante sana kwa kutumia muda wako kusoma Makala hii.
 Usisite kutupatia mchango wako wa mawazo au kama unaswali lolote usisite kuuliza, tutakupatia majibu sahihi. Usisahau kumshirikisha mwenzako ili naye apate kuelimika.


 


   
                                                                                                                                        

Comments